Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amewasha umeme kwa mara ya kwanza katika Kata ya Upendo mtaa wa Lumwago uliyopo katika Halmashauri ya Mji wa Mafinga, Mkoa wa Iringa.
Uzinduzi huo uliofanyika mbele ya mamia ya wananchi wa mtaa wa Lumwago ambao walikuwa na furaha baada ya kuona umeme huo umewaka kwa mara ya kwanza
Waziri Kalemani alifanya uzinduzi huo akiwa katika ziara ya kazi mkoani Iringa wakati wa kukagua miradi ya umeme inayotekelezwa na REA awamu ya tatu.
Awali, akiongea na wananchi Dkt. Kalemani alisema kuwa wananchi zaidi ya 200 wataanza kupata umeme kufuatia tukio la kurasimishwa kuwashwa kwa nishati hiyo Lumwago.
“Tunatoa kipaumbele chetu kwa sasa kwani ni kuhakikisha kwamba wananchi wengi wanapata umeme na huduma hiyo inakuwa ya uhakika,” alisema Dkt. Kalemani.
Akifafanua zaidi, alisema kuwa, Serikali imeanzisha harakati za kufanya ukaguzi kwenye utekelezaji wa Miradi yote ya umeme mkoani humo.
Aidha, alitumia fursa hiyo kuwataka viongozi wa Halmashauri mbalimbali za vijiji kote nchini, kuhakikisha wanajiandaa kwa ajili ya kuunganishiwa umeme katika taasisi zote za umma zikiwemo Shule, Vituo vya Afya, Miradi ya Maji, Masoko na nyinginezo.
Vilevile, alikumbushia umuhimu wa kila mmoja kuhakikisha baada ya kuunganishiwa umeme katika eneo lake anakumbuka kulipa bili za huduma hiyo muhimu.
“Usipolipa,Serikali itakukatia umeme hivyo kurudisha nyuma maendeleo yako,” alisisitiza.
Jambo jingine ambalo Waziri Kalemani alisisitiza ni kwa wakandarasi kuhakikisha wanawagawia bure wateja 200 wa kwanza watakaojitokeza kuunganishiwa umeme wa REA kifaa cha Umeme kinachokulikana kwa jina la UMETA kama ilivyoelekezwa na Serikali na siyo vinginevyo.
Hapo awali mbunge wa jimbo la Mafinga Mjini Mh.Cosato Chumi pamoja na kupongeza jitihada ambazo Wizara ya nishati imekuwa ikifanya nchi nzima katika kuhakikisha huduma ya umeme inapatikana katika maeneo mbalimbali, pia alimwomba Waziri Kalemani kulipa upendeleo jimbo hilo kwa kuwa ndio kitovu cha uchumi wa viwanda mkoani Iringa.
“Mheshimiwa nikuombe utusaidia kwenye vijiji vilivyobaki katika jimbo langu kwasasababu wananchi wangu niwachapakazi na wapenda maendeleo” alisema Chumi.
Mh. Chumi aliendelea kumwambia waziri kuwa jimbo la Mafinga Mjini ni moja kati ya maeneo ambayo yana viwanda vingi ambavyo vinasaidia kukuza uchumi wa nchi pamoja na kuongeza ajira kwa watanzania wanaoishi katika jimbo hilo.
“Hapa tunazaidi ya viwanda arobaini vya mazao ya miti na tunaviwanda vingine vingi na viwanda vyote hivi vinatumia nisharti ya umeme hivyo naomba nitoe rai kuwa Mji wa Mafinga unahitaji sana huduma ya nishati hii kwa kiasi kikubwa” alisema Chumi.
Mafinga Town.
Postal Address: Po.Box 76 Mafinga
Simu: +255 262 772 393
Mobile: 026-2772393
Barua Pepe: td@mafingatc.go.tz
Copyright ©2018 Mafinga Town Council . All rights reserved.