Madaktari Bingwa wa Macho kutoka Hospitali ya Rufaa Mbeya, Iringa pamoja na hospitali ya kilutheri ilembula wanaendelea na Utoaji wa Huduma za Upimaji na Matibabu ya Macho kwa Wagonjwa wa Hospitali ya Mji Mafinga na Huduma hiyo inatolewa kuanzia tarehe 24/11/2025 Mpaka tarehe 28/11/2025.

Akizungumza katika Ofisi za Hospitali ya Mji Mafinga Mratibu wa Shughuli za Macho Ndugu Robert Michael amesema lengo la Ziara hiyo ya Madaktari Bingwa ni kutoa Huduma za Upimaji na Upasuaji mkubwa wa Mtoto wa Jicho pia kutoa Elimu kwa Wagonjwa jinsi ya kutunza Macho na Kufanya uchunguzi mkubwa wa ndani kuhusu matatizo ya Macho.
"Watu wengi Wana shida ya magonjwa ya Macho hivyo tunapambana kutoa Elimu ili waweze kupima Afya ya Macho angalau mara Moja kwa Mwaka pia watu waepuke Tiba Asili au kununua dawa bila kupata Ushauri wa Daktari Kwa sababu inaweza kusababisha Upofu hivyo ni vyema kupata Matibabu katika Hospitali yenye Madaktari Bingwa wa Macho". amesema Ndugu Robert.

Naye Daktari Bingwa wa Macho kutoka Hospitali ya kilutheri Ilembula Dkt.Shaha Pelapela amesema zoezi la Upimaji na Utoaji Matibabu limepokelewa vizuri na Wagonjwa wengi wamefika Hospitali ya Mji Mafinga kwa ajili ya kupata Huduma na Idadi kubwa ya Wazee wanasumbuliwa na Mtoto wa Jicho,Vijana wengi wanahitaji Huduma ya Miwani na kwa Watoto wanasumbuliwa na Macho kwa sababu ya kimazingira kama vumbi.
"Watu Wazingatie Kanuni za Afya na jinsi ya kutunza Macho kama kunawa uso kwa Maji Safi kutoka bombani pia ni vyema watu wawe na Utaratibu wa kupima Afya ya Macho ili kupunguza Magonjwa ya Macho." Amesema Dkt.Shaha.

Pamoja na hayo mmoja wa Wagonjwa waliofika Hospitali ya Mji Mafinga kwa ajili ya kupata Matibabu Mzee Alex Kiyeyeu Mkazi wa Kijiji Cha Itona Mufindi amewapongeza Uongozi wa Hospitali kwa kuratibu vyema zoezi la Upimaji Macho kwa sababu ya Huduma nzuri waliyopewa Wagonjwa hivyo anawashauri Watu wenye Matatizo ya Macho kufika katika Hospitali ya Mji Mafinga ili waweze kupata hiyo Huduma.
Nasri Mwinyi
Afisa Habari - Mafinga TC
Mafinga Town.
Postal Address: Po.Box 76 Mafinga
Simu: +255 262 772 393
Mobile: 026-2772393
Barua Pepe: td@mafingatc.go.tz
Copyright ©2018 Mafinga Town Council . All rights reserved.